Ad Code

Masomo ya Misa Juni 24,2022; Ijumaa: Juma La 12 La Mwaka

SOMO 1: Eze. 34:11-16

Bwana Mungu asema hivi: “Tazama, mimi mwenyewe, naam, mimi, nitawatafuta kondoo zangu, na kuwaulizia. Kama vile mchungaji atafutavyo kondoo zake, siku ile anapokuwa kati ya kondoo zake waliotawanyika; ndivyo nitakavyowatafuta kondoo zangu; nami nitawaokoa katika mahali pote walipotawanyika, katika siku ya mawingu na giza. Nami nitawatoa katika watu wa mataifa na kuwakusanya katika nchi zote; nami nitawarudisha katika nchi yao wenyewe; nami nitawalisha juu ya milima ya Israeli, kando ya mifereji ya maji; na katika mahali pote pa nchi panapokaliwa na watu. Nami nitawalisha malisho mema, na juu ya milima ya mahali palipoinuka pa Israeli litakuwa zizi lao; huko watalala katika zizi jema; nao watakula malisho mema juu ya milima ya Israeli. Mimi mwenyewe nitawalisha kondoo zangu, nami nitawalaza, asema Bwana Mungu. Nami nitawatafuta waliopotea, nitawarudisha waliofukuzwa, nitawafunga waliovunjika, nitawatia nguvu wagonjwa; nao wanono na wenye nguvu nitawaharibu; nitawalisha hukumu.”

Wimbo Wa Katikati: Zab. 23

  1. Bwana ndiye mchungaji wangu,
    Sitapungukiwa na kitu;
    Katika malisho ya majani mabichi hunilaza,
    Kando ya maji ya utulivu huniongoza.

(K) Bwana ndiye mchungaji wangu sitapungukiwa na kitu.

  1. Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza
    Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake.
    Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti,
    Sitaogopa mabaya;
    Kwa maana Wewe upo pamoja name,
    Gongo lako na fimbo yako vyanifariji. (K)
  2. Waandaa meza mbele yangu,
    Machoni pa watesi wangu.
    Umenipaka mafuta kichwani pangu,
    Na kikombe change kinafurika. (K)
  3. Hakika wema na fadhili zitanifuata
    Siku zote za maisha yangu;
    Nami nitakaa nyumbani mwana Bwana milele. (K)

SOMO 2: Rum. 5:5-11

Pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yetu na Roho Mtakatifu tuliyepewa sisi. Kwa maana hapo tulipokuwa hatuna nguvu, wakati ulipotimia, Kristo alikufa kwa ajili ya waovu. Kwa kuwa ni shida mtu kufa kwa ajili ya mtu mwenye haki; lakini yawezekana mtu kuthubutu kufa kwa ajili ya mtu aliye mwema. Basi Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi. Basi zaidi sana tukiisha kuhesabiwa haki katika damu yake, tutaokolewa na ghadhabu kwa yeye. Kwa maana ikiwa tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kwa mauti ya Mwana wake; zaidi sana baada ya kupatanishwa tutaokolewa katika uzima wake. Wala si hivyo tu, ila pia twajifurahisha katika Mungu kwa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa yeye sasa tumeupokea huo upatanisho.

INJILI: Lk. 15:3-7

Yesu aliwaambia mfano huu, “Ni nani kwenu, mwenye kondoo mia, akipotewa na mmojawapo, asiyewaacha wale tisini na kenda nyikani, aenda akamtafute yule aliyepotea hata amwone? Naye akiisha kumwona, humweka mabegani pake akifurahi. Na afikapo nyumbani kwake, huwaita rafiki zake na jirani zake,” akawaambia, “Furahini pamoja nami, kwa kuwa nimekwisha kumpata kondoo wangu aliyepotea. “ Nawaambia, “Vivyo hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na kenda ambao hawana haja ya kutubu.”

TAFAKARI
MOYO ULIOJAA NEEMA ZA MUNGU: Leo Mama Kanisa anatualika kuadhimisha pamoja naye sherehe ya Moyo Mtakatifu wa Yesu. Tunautafakari moyo huu kwani ni chemichemi ya neema za Mungu, na unatusaidia kutambua madhumuni ya Mungu Baba. Maneno ya kinabii ya Ezekieli yanatuonjesha utajiri wa moyo huu. Mungu wetu ni Mungu wa Huruma; ‘naahidi kuwatafuta na kuwakusanya tena.’ Ni Mkombozi; atawaokoa popote walipotawanyika. Ni Mungu anayewajali wasiokuwa na hifadhi; ‘nitawarudisha katika nchi yao wenyewe.’ Ni Mungu anayewajali watu wake; ‘nitawalisha juu ya milima ya Israeli.’ Ni Mungu anayeponya, kupatanisha na kufariji; ‘nitawalaza, nitawafunga waliovunjika, nitawatia nguvu wagonjwa.’ Zaburi inamsifu Mungu kama Mchungaji anayewatosheleza kondoo wake.
Injili anaonyesha jinsi gani Mungu anavyomthamini kila mmoja kwa nafasi yake. Mchungaji yupo tayari kuwaacha wengine wote na kumfuata mmoja aliepotea na aliye hatarini, na inakuwa furaha anapopatikana.

SALA: Ee Yesu, utujalie kufahamu utajiri wa Moyo wako mtakatifu, na utugawie neema zake.

Post a Comment

0 Comments